Tuesday, August 28, 2012

Hii kali - Wanawake Togo wasusia ngono kudai Mageuzi

 Isabelle Ameganvi anasema kususia ngono kutasaidia wanawake kusikika 



Wanawake nchini Togo, wametakiwa kususia kitendo cha ndoa kuanzia Jumatatu wiki hii kama njia ya kushinikiza serikali kuleta mageuzi. Kampeini hiyo yenye kauli mbiu ''Juhudi za kuokoa Togo'' imeanzishwa kwa ushirikiano na mashirika tisa ya kijamii pamoja na vyama saba vya upinzani pamoja na vyama vingine vya kijamii.
Kiongozi wa upinzani, Isabelle Ameganvi alisema kuwa kususia ngono huenda ndio itakuwa silaha inayofaa kuweza kuleta mageuzi ya kisiasa. Muungano wa vyama hivyo pamoja na mashirika yasiyo ya kijamii unataka Rais Faure Gnassingbe, ambaye familia yake imeshikilia madaraka kwa miaka mingi waweze kuondoka mamlakani.

"tuna njia nyingi za kuwashinikiza wanaume kuelewa tunachotaka sisi wanawake'' alisema bi Ameganvi, kiongozi wa tawi la wanawake la muungano huo.

Vurugu Togo
Togo imekuwa ikiongozwa na familia moja kwa zaidi ya miaka arobaini. Rais Faure Gnassingbe alichukua mamlaka mnamo mwaka 2005 kufuatia kifo cha babake Gnassingbe Eyadema, aliyetawala Togo kwa miaka 38. Rais alichaguliwa kwa muhula mwingine mnamo mwaka 2010.

Alisema kuwa yeye ameweza kushawishiwa na mgomo sawa na huo nchini Liberia mwaka 2003, ambao walitumia njia ya kususia ngono kushinikiza amani. "ikiwa wanaume watakataa kusikia kilio chetu, tutalazimika kufanya maandamano ambayo yatakuwa makali zaidi kuliko mbinu hii ya kususia ngono.'' aliongeza bi Ameganyi.

Mgomo huo ulitangazwa katika mkutano wa hadhara mnamo siku ya Jumamosi mjini Lome, na ambao ulihudhuriwa na maelfu ya watu. Mkutano huo ulifanyika kupinga mabadiliko ya hivi karibuni yaliyofanywa ambayo wakereketwa wanasema kuwa yatarahisisha ushindi wa chama tawala cha Gnassingbe kuweza kwenye uchaguzi wa bunge utakaofanyika mwezi Oktoba.

Wanaharakati wanasema kuwa mgomo huo utashinikiza wanaume ambao hawajihusishi na mchakato wa kisiasa kuweza kuhakikisha malengo yake yanatimizwa ambayo ni pamoja na kukomeshwa kwa utawala wa Rais usio na kikomo. Mapema mwezi huu, waandamanaji wanaopinga utawala wa Rais Gnassingbe walitawanywa na polisi kwa kutumia gesi ya kutoa machozi na wengine zaidi ya mia moja wakakamatwa.

Source: BBC

No comments: