Thursday, October 11, 2012

China yahusishwa kuchochea ujangili wa tembo katika hifadhi za Tanzania

Bendera ya China
BAADHI ya mataifa ya Mashariki ya mbali ikiwamo China yamedaiwa kuchochea kwa kiasi kikubwa kuendelea kwa vitendo vya ujangili katika mbuga za wanyama nchini kutokana na nchi hizo kuruhusu biashara ya pembe za ndovu. Naibu Waziri wa Mali Asili na Utalii, Lazaro Nyalandu alisema jana kuwa mbali na China mataifa mengine ni  yanayochochea biashara  ya pembe ni Hong Kong, Japan na Korea Kusini. Mbali na kuwapo kwa hali hiyo, Serikali imesema pi inafahamu mtandao wa kimataifa unaolizalisha silaha kwa ajili ya kufadhili vitendo vya kijangili kwenye mbuga za wanyama nchini Tanzania.

Nyalandu alisema hayo alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuzungumzia pamoja na mambo mengine, kongamano la utalii linalotarajiwa kufanyika wiki ijayo mkoani Arusha.
Ukuta mkuu wa China
mojawapo ya vivutio vikubwa vya utalii vya China
"Sisi tumefanya mapitio tukabaini vyanzo vya tatizo hili…tumegundua wateja wengi wa meno ya tembo wanatoka China. Kila msichana nchini China anavaa cheni iliyotengenezwa kwa meno ya tembo na matokeo yake, imepandisha gharama ya kilo moja ya meno hayo kutoka Dola 100  hadi Dola 1,000, hivi vyote ni vichochezi," alisema na kuongeza: "Hebu fikiria, China yenyewe ina watu zaidi ya bilioni 1, sasa jumlisha na wateja wengine kutoka Japan, Korea Kusini, Hong Kong na nchi zingine za Mashariki ya mbali."

Kutokana na ukubwa wa tatizo hilo, Nyalandu alisema Serikali imeuomba upya Umoja wa Mataifa kuuza akiba yake ya meno ya tembo yaliyotaifishwa ili kupata fedha za kuimarisha ulinzi kwa lengo la kumaliza tatizo hilo la ujangili.

"Tukifanikiwa azma hiyo tutahitaji kupata ushirikiano wa karibu toka Jumuiya za Kimataifa wakiwamo polisi wa kimataifa ‘interpol’ na nchi wahisani ili kukamata bidhaa zake yakiwamo meno ya tembo yaliyosafirishwa kimagendo," alisema.

Mh. Lazaro Nyalandu
Naibu waziri wa wizara ya
maliasili na utalii
Nyalandu alisema kuwa vitendo vya ujangili vinaendelea kuwa tishio kwa mali asili ya taifa hivyo kunahitajika mkakati wa kukabiliana nao. Naibu Waziri Nyalandu alikiri ugumu uliopo wa kukabiliana na wimbi la vitendo vya kijangili ambao alisema unaziandama karibu nchi nyingi za Afrika, lakini alisisitiza kuwa Serikali imedhamiria kuusambaratisha mtandao huo kwa vile wahusika wake tayari wanatambulika.

“Serikali inafahamu mitandao yote inayojihusisha na biashara haramu ya ujangili. Tunawafahamu wale wanatumika kuingiza silaha nchini na kufanya uhalifu. Lakini pia tunafahamu nchi duniani ambako meno haya ya tembo yanaenda na jinsi gani yanaenda na tumeiomba dunia tushirikiane katika hili,” alisema Naibu Waziri huyo.

Alisema kuwa tatizo la ujangili wa meno ya tembo haliwezi kukabiliwa na nchi moja kwani limechukua sura ya kimataifa hivyo ni wajibu wa kila nchi kushirikiana na taifa lingine kufifisha hujuma zinazoendeshwa na mitandao hiyo. “Nenda Kenya hali ni ile ile, sasa sisi tunasema kuwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama viko tayari kukabiliana na ujangili huu na tunaomba wenzetu pia tushirikiane,” alisisitiza Nyalandu.

Naibu Waziri Nyalandu alisema kuwa mkutano wa kimataifa uliofanyika huko Doha chini ya mwamvuli wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na utalii (UNTO) ulizima jaribio la Tanzania kuuza meno hayo ya tembo, lakini sasa Serikali inakusudia kutumia kikao kijacho kitakachofanyika Bangkok kupenyeza ushawishi wake ili iruhusiwe kuuza meno hayo.

Wakati huohuo Wizara ya Mali ya asili na Utalii itakuwa mwenyeji wa Kongamano la Kimataifa linalotarajiwa kufanyika jijini Arusha kuanzia Oktoba 15 mwaka huu. Kongamano hilo ambalo litahusu usimamizi wa utalii endelevu katika hifadhi ya taifa na linatarajiwa kuhudhuriwa na wajumbe 412 kutoka mataifa 40 ya Afrika.

SOURCE YA HABARI HII: http://www.mwananchi.co.tz

No comments: