Wednesday, September 12, 2012

Jeshi lawekwa katika hali ya tahadhari nchini Afrika Kusini


Wanajeshi wa Afrika Kusini .
Kambi za jeshi nchini Afrika Kusini zimewekwa katika hali ya tahadhari ikiwa ni mara ya kwanza tangu kuanza kwa utawala wa kidemokrasia nchini humo . Hatua hiyo inajiri wakati mwanasiasa mwenye utata , Julius Malema akijiandaa kuwahutubia wanajeshi wanaonung'unika nje ya mji wa Johannesburg

Imeonekana kuwa hatua isiyokuwa ya kawaida.
Wizara ya ulinzi ya Afrika Kusini imethibitisha kuwa kambi zote za kijeshi zimewekwa katika hali ya tahadhari kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1994. Yote haya ni kutokana na mpango wa Julius Malema kutaka kuzungumza na baadhi ya wanajeshi.
Bwana Malema ni mwanasiasa anayeibua mgawanyiko hapa. Hivi maajuzi alifukuzwa kutoka chama cha ANC na kwa sasa anafanyiwa uchunguzi kuhusiana na kashfa ya ufisadi.

Lakini hajaondoka ANC kimya kimya. Badala yake ametumia mauaji ya hivi maajuzi katika mgodi wa marikana kuanzisha kampeni kali dhidi ya mabepari nchini Afrika Kusini na kutaka yafanyike mapinduzi ya kiuchumi. Wengi wanamshutumu kwa kuhusika na ubinafsi mbaya wa kisiasa, lakini Malema anapokea uungwaji mkubwa kutoka kwa jamii za watu maskini na kimya cha serikali ni ishara tosha kuwa imeshindwa kukabiliana naye.

Manung'uniko ya wanajeshi ni fursa nyingine kwa Malema kuonyesha ubabe wake na hali ni tete nchini Afrika Kusini. Hofu iliyopo ni kwamba migomo huenda ikaenea zaidi na kwamba serikali kwa sasa inazingirwa na migogoro ya ndani huku baadhi ya mirengo serikalini ikipanga njama ya kumtimua madarakani Rais Jacob Zuma.

Source: BBC Swahili.

No comments: