Wednesday, September 26, 2012

Maelfu waomboleza kifo cha Omran Ben Shaaban, Ndio yule anayeaminika kumkamata Kanali Muammar Gaddafi


Waombolezaji wakiwa wamebeba jeneza
lenye mwili wa Omran Ben Shaaban
Zaidi ya watu 10,000 nchini Libya walikusanyika kuomboleza kifo cha mmoja wa waasi waliosifika kwa kumkamata hayati Muammar Gaddafi mwaka jana. Omran Ben Shaaban alifariki Jumanne iliyopita baada ya kutekwa , kupigwa risasi na kuteswa na wafuasi wa hayati Gaddafi.

Mwili wa kijana huyo aliyekuwa na umri wa miaka 22, ulipelekwa nyumbani kwao mjini Misrata kwa mazishi. Serikali ilisema kuwa itampa mazishi ya kishujaa kijana huyo huku kukiwa na wito wa serikali kulipiza mauaji yake. Omran Ben Shaaban alikamatwa na watu waliokuwa wamejihami mnamo mwezi Julai, na kuzuiliwa kwa siku 50 mjini Bani Walid, ilipokuwa ngome ya Gaddafi Kusini Mashariki mwa Tripoli. Aliachiliwa wiki jana baada ya juhudi za upatanishi kufanywa na kiongozi wa mpito wa nchi hiyo Mohammed Magarief.

Bwana Omran Ben Shaaban aliwasili mjini Misrata akiwa na alama za mateso pamoja na alama ya risasi kwenye uti wake wa mgongo. Alipelekwa mjini, Paris kwa matibabu ingawa alifariki baadaye. Omran Ben Shaaban alianza kujulikana tarehe 20 mwezi Oktoba mwaka jana, wakati alipoonekana katika sehemu alikokamatwa marehemu Kanali Gaddafi mjini Sirte. Wengi wameomboleza kifo chake, aliyetambulika kama shujaa huku serikali ikisema itafanya juhudi za kuwasaka watesi wake na kuwahukumu.

No comments: